Andiko:
“Ufunuo 12:11 – Nao wakamshinda kwa damu ya Mwanakondoo na kwa neno (logos) la ushuhuda wao…”
Tafakari:
Katika maandiko ya asili, neno lililotumika hapa ni logos la Kiyunani, ambalo halimaanishi tu “neno lililosemwa,” bali pia linaonyesha kanuni ya kimungu iliyo wazi na thabiti. Kwa maneno mengine, ushindi wa waamini haukutokana na maneno ya kawaida, bali ni ukiri wenye msingi katika kanuni za Mungu.
Aidha, Mithali 18:21 inasema: “Mauti na uzima hu katika uwezo wa ulimi.” Katika Kiebrania, neno “ulimì” limetokana na neno lashon ambalo si tu kiungo cha mwili, bali ni ishara ya mamlaka ya kuamua hatima kwa kusema. Hivyo, kila ukiri wa mtu unaweza kuwa mbegu ya uhai au hukumu ya mauti.
Yesu mwenyewe alipojaribiwa jangwani (Mathayo 4:4), alitumia neno gegraptai – “Imeandikwa.” Hapa si kutaja tu andiko, bali ni kulisema kama tangazo la mamlaka. Kimsingi alisema: “Neno hili limekwisha kuamuliwa na halibadiliki.”
Hii inatufundisha kwamba ukiri sahihi si mawazo yetu binafsi, bali ni kurudia kile Mungu amesema tayari. Tunapolingana na Neno lake, ukiri wetu unakuwa ni silaha ya kiroho na tangazo la ushindi.
Nugget ya Dhahabu:
“Ukiri sahihi si maneno ya kawaida; ni logos ya ushindi inayojengwa juu ya kile Mungu amesema.”
OMBA NAMI;
Baba wa mbinguni, nakushukuru kwa nguvu ulizoziweka katika ulimi wangu. Nisaidie kila siku niwe na ukiri unao lingana na Neno lako, siyo hofu wala mashaka. Ninakiri ushindi, afya, amani, na baraka katika jina la Yesu. Amina.
Leave a comment