Katika safari yao kuelekea Kanaani, Musa hakutamani tu kufika kwenye nchi ya ahadi bali alitamani uwepo wa Mungu zaidi ya ahadi hiyo. Alitambua kuwa bila Mungu, hata ahadi nzuri ya nchi yenye maziwa na asali haina maana. Uwepo wa Mungu ndio ulioleta utofauti kati yao na mataifa mengine.
Musa akamwambia, “Usipokwenda pamoja nasi, usitutoe hapa.”
Kutoka 33:15 (SUV)
Hata leo, kuna vitu vingi vinavyoweza kutuvutia mafanikio, mali, heshima, vipawa n.k lakini hakuna kitu kinachoweza kuchukua nafasi ya uwepo wa Mungu. Uwepo Wake huleta amani, huyapa maisha maana, ushindi, uelekeo na utukufu.
Wengi huomba vitu kutoka kwa Mungu lakini wachache humtamani Mungu Mwenyewe. Musa anatufundisha njia bora kumtamani Mungu kuliko zawadi na vipawa vitakavyo kwake. Kama uwepo wa Mungu uko pamoja nawe, haijalishi mahali ulipo au unakopitia, uko salama.
NUGGET YA DHAHABU:
“Mungu hupenda sana watu wake kuwa na vipawa vitokavyo kwake Ila hufurahia zaidi ushirika na mwanadamu ambao hualika uwepo wake hapa Duniani. Mtafute Yeye zaidi ya kitu kingine chochote.”
Shallom!
OMBA NAMI
Baba, ninakutafuta zaidi ya zawadi zako. Ninakutamani Wewe, uwepo Wako, na ushirika na Roho Mtakatifu. Nisamehe kwa nyakati nilizoweka vitu vikachukua nafasi ya uwepo wako. Najua kama uko pamoja nami, nina kila kitu. Katika jina la Yesu, Amen
Leave a comment